Waziri wa Uchukuzi, Dk. Harrison Mwakyembe
Waziri wa Uchukuzi, Dk. Harrison Mwakyembe, ametoa siku
90 kwa matrekta yote yanayoingia Bandari ya Dar es Salaam kubeba
makontena kuacha mara moja.
Dk. Mwakyembe ametoa agizo hilo jana wakati akifungua Maonyesho ya
Kilimo ya Nanenane yanayofanyika kikanda jijini Mbeya yakiwa na
kaulimbiu ya “Zalisha Mazao ya Kilimo na Mifugo kwa kulenga Mahitaji ya
Soko”.
“Matrekta mengi nimeyaona bandarini yakitumika kubeba mizigo, kwa mfano
makontena, natoa miezi mitatu kuanzia sasa matrekta yote yanayotumika
bandarini yaende yanakohitajika kwenye kilimo. Ikifika Oktoba 30
mwaka huu matrekta sitaki kuyaona bandarini,”alisema Dk. Mwakyembe.
Asema serikali imeweza kufuta ushuru wa zana za kilimo kama matrekta chini ya kampeni ya Kilimo
Kwanza, lakini matrekta mengi yaliyoingizwa kuwezesha kilimo kukua yameishia kubeba mizigo bandarini.
Alisema uzalishaji wa mazao ya kilimo na mifugo katika mikoa ya Kanda ya Nyanda za Juu Kusini ipo chini
sana ikilinganishwa na viwango vya utafiti, mfano hekta moja ya zao la
mahindi inazalisha wastani wa tani tatu lakini utafiti unaonesha kwamba
hekta moja ya zao la mahindi inaweza kuzalisha wastani wa tani saba za
mahindi.
Alisema kwa upande wa maziwa wastani wa uzalishaji kwa ng’ombe mmoja kwa
siku ni lita saba wakati kiwango kinachotakiwa kuzalishwa ni lita 20
kwa ng’ombe kwa siku.
Dk. Mwakyembe alisema upo umuhimu mkubwa wa kuyaongezea thamani mazao
kwa njia ya viwanda vidogovidogo ili yauzike kwa haraka na kwa bei nzuri
zaidi na kukidhi matakwa mbalimbali ya soko.
Aliongeza kuwa katika mwaka huu wa fedha serikali imeelekeza nguvu kubwa
kupeleka umeme kwa wakulima kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA).
Alisema katika utekelezaji wa mradi huo vijiji 590 vya mikoa ya Mbeya,
Katavi, Ruvuma, Rukwa, Njombe na Iringa vimetengewa kiasi cha Sh.
bilioni 162.5 kwa miradi ya umeme ambayo utekelezaji wake
umeshaanza kwa kazi ya uteuzi wa makandarasi ambao wanatakiwa kuanza kazi ya usambazaji umeme mwezi Oktoba mwaka huu.
Alisema miradi hiyo ya umeme itachochea uanzishwaji wa viwanda vidogo
vidogo vijijini vitakavyoongeza thamani ya mazao ya wakulima na kwamba
serikali imechukua hatua ya ziada ya kupunguza gharama za kufungiwa
umeme vijijini kwa asilimia 70.
Aliongeza kuwa mikoa ya Nyanda za Juu Kusini imetengewa zaidi ya Sh.
bilioni 5 kwa kazi ya kukarabati barabara vijijini, matumizi ya fedha
hizo yakisimamiwa vizuri itasaidia kuleta mabadiliko katika kusafirisha
mazao vijijini.
Kuhusu sekta ya uchukuzi wa anga, reli na majini, alisema serikali
inaendelea kuimarisha reli ya TAZARA kwa ushirikiano wa serikali zetu
mbili za Tanzania na Zambia, tuko kwenye maandalizi ya ujenzi wa reli
kutoka Uyole kwenda Mgodi wa Makaa ya Mawe Kiwira, kuunganisha Tunduma na bandari ya Kasanga katika Ziwa Tanganyika.
Kazi nyingine ni kuimarisha reli kutoka Tabora hadi Mpanda na
kuiendeleza reli hiyo hadi bandari ndogo ya Kalema kwenye Ziwa
Tanganyika pamoja na ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami kwenye
mikoa ya Ruvuma na Iringa, na barabara ya kuunganisha mikoa ya Rukwa,
Katavi na Mbeya.
CHANZO: NIPASHE JUMAPILI
Categories: