[employment%255B2%255D.jpg]



IMEANDIKWA NA MAKIRITA AMANI WA AMKA MTANZANIA
Tunaishi kwenye kipindi chenye changamoto nyingi sana hasa linapkuja swala la ajira. Katika swala la ajira kuna makundi matatu, kuna walioajiriwa, kuna waliojiajiri na kuna ambao hawapo kwenye ajira kabisa ila bado wanatengeneza fedha.
  Walioajiriwa ni wale wanaofanya kazi na kulipwa.  Waliojiajiri ni wale waliotengeneza ajira zao wenyewe na wanaweza kuwa wameajiri watu wengine. Ambao hawako kwenye ajira kabisa ni wale ambao wameshatengeneza mifumo ambayo inawaingizia fedha bila ya wao kufanya kazi kubwa. Yaani mtu anaweza kulala mwezi mzima na bado fedha zinaingia.
employment
  Nafasi za kuajiriwa kwa sasa zimekuwa chache sana na hata ajia zenyewe zimekuwa mzigo sana kwa waajiriwa. Kutokana na hayo watu wengi wanafikiri kujiajiri ndio suluhisho la tatizo hili la ajira.
  Kujiajiri kunaweza kuwa suluhisho la tatizo la ajira kama umejipanga kweli kujiajiri(soma; kama una tabia hizi usijaribu kujiajiri) Ila pia kwenye kujiajiri kuna changamoto na kama hujajipanga vizuri hali inaweza kuwa mbaya kuliko hata kwenye ajira.
  Unapokuwa kwenye ajira mara nyingi kuna saa maalumu za kufanya kazi, na mara nyingi huwa masaa nane mpaka kumi kwa siku. Unapokuwa umejiajiri mwenyewe unaweza kujikuta unafanya kazi zaidi ya masaa 10 kwa siku na mara nyingi ndivyo inavyokuwa. Wewe ndio unakuwa bosi na wewe ndio muajiriwa wa kwanza, hata kama una watu umewaajiri.
  Watu wengi waliojiajiri wao wanakuwa ndio kila kitu kwenye ajira zao, kama asipokwenda kazini kwa siku moja tu, madhara yanakuwa makubwa sana kwenye kazi yake.
  Kama umejiajiri na kazi yako haiwezi kwenda bila ya wewe basi huna tofauti na alieajiriwa na huenda wewe ukawa unafanya kazi ya kukuumiza zaidi ya hata alieajiriwa. Unaweza kuwa unapata kipato kikubwa zaidi ya alieajiriwa ila kama unafanya kazi masaa 14 kwa siku(unaondoka nyumbani saa 12 asubuhi unarudi saa 2 usiku) unafikiri umepata uhuru wa ajira hapo? Je unaweza kufanya kazi hiyo kwa muda gani kabla mwili haujachoka na kushindwa kufanya hivyo? Je umeshafikiria utafanya nini pale utakapokosa nguvu ya kufanya unachofanya?
  Kama unataka kujiajiri ama tayari umejiajiri weka mipango ya kutokuwa kwenye ajira kabisa. Weka mpango labda baada ya miaka kumi ya kufanya kazi masaa14 kwa siku utakuwa umeshatengeneza mfumo wa kukutengenezea fedha ambao hautakuhitaji tena kufanya kazi masaa hayo. Huwezi kufanya kazi unayoifanya kwa miaka yako yote unayoishi, kuna wakati utachoka. Lazima uweke mipango ya kujua utaishi vp pale utakapochoka.
  Vinginevyo ukifika wakati wa kustaafu utastaafu kama waliokuwa wameajiriwa na wao watakuwa na afadhali kuliko wewe kwa sababu kuna sehemu ya fedha wanaweza kupata kama mafao.

Categories:

Leave a Reply