IMEANDIKWA NA MAKIRITA AMANI WA AMKA MTANZANIA
Tunaishi kwenye kipindi chenye changamoto nyingi sana
hasa linapkuja swala la ajira. Katika swala la ajira kuna makundi
matatu, kuna walioajiriwa, kuna waliojiajiri na kuna ambao hawapo kwenye
ajira kabisa ila bado wanatengeneza fedha.
Walioajiriwa ni wale wanaofanya kazi na kulipwa. Waliojiajiri ni wale
waliotengeneza ajira zao wenyewe na wanaweza kuwa wameajiri watu
wengine. Ambao hawako kwenye ajira kabisa ni wale ambao wameshatengeneza
mifumo ambayo inawaingizia fedha bila ya wao kufanya kazi kubwa. Yaani
mtu anaweza kulala mwezi mzima na bado fedha zinaingia.
Nafasi za kuajiriwa kwa sasa zimekuwa chache sana na hata ajia zenyewe
zimekuwa mzigo sana kwa waajiriwa. Kutokana na hayo watu wengi
wanafikiri kujiajiri ndio suluhisho la tatizo hili la ajira.
Kujiajiri kunaweza kuwa suluhisho la tatizo la ajira kama umejipanga kweli kujiajiri(soma; kama una tabia hizi usijaribu kujiajiri) Ila pia kwenye kujiajiri kuna changamoto na kama hujajipanga vizuri hali inaweza kuwa mbaya kuliko hata kwenye ajira.
Unapokuwa kwenye ajira mara nyingi kuna saa maalumu za kufanya kazi, na
mara nyingi huwa masaa nane mpaka kumi kwa siku. Unapokuwa umejiajiri
mwenyewe unaweza kujikuta unafanya kazi zaidi ya masaa 10 kwa siku na
mara nyingi ndivyo inavyokuwa. Wewe ndio unakuwa bosi na wewe ndio
muajiriwa wa kwanza, hata kama una watu umewaajiri.
Watu wengi waliojiajiri wao wanakuwa ndio kila kitu kwenye ajira zao,
kama asipokwenda kazini kwa siku moja tu, madhara yanakuwa makubwa sana
kwenye kazi yake.
Kama umejiajiri na
kazi yako haiwezi kwenda bila ya wewe basi huna tofauti na alieajiriwa
na huenda wewe ukawa unafanya kazi ya kukuumiza zaidi ya hata
alieajiriwa. Unaweza kuwa unapata kipato kikubwa zaidi ya alieajiriwa
ila kama unafanya kazi masaa 14 kwa siku(unaondoka nyumbani saa 12
asubuhi unarudi saa 2 usiku) unafikiri umepata uhuru wa ajira hapo? Je
unaweza kufanya kazi hiyo kwa muda gani kabla mwili haujachoka na
kushindwa kufanya hivyo? Je umeshafikiria utafanya nini pale utakapokosa
nguvu ya kufanya unachofanya?
Kama
unataka kujiajiri ama tayari umejiajiri weka mipango ya kutokuwa kwenye
ajira kabisa. Weka mpango labda baada ya miaka kumi ya kufanya kazi
masaa14 kwa siku utakuwa umeshatengeneza mfumo wa kukutengenezea fedha
ambao hautakuhitaji tena kufanya kazi masaa hayo. Huwezi kufanya kazi
unayoifanya kwa miaka yako yote unayoishi, kuna wakati utachoka. Lazima
uweke mipango ya kujua utaishi vp pale utakapochoka.
Vinginevyo ukifika wakati wa kustaafu utastaafu kama waliokuwa
wameajiriwa na wao watakuwa na afadhali kuliko wewe kwa sababu kuna
sehemu ya fedha wanaweza kupata kama mafao.
Categories: