Leo tutaangalia jinsi ambavyo maamuzi mazuri unayoyaamua katika maisha yako yanavyokupa ujasiri wa kusonga mbele katika kufikia malengo uliyojiwekea.
Kumbuka kama unataka kuwa mtu fulani katika jamii au kuwa kiongozi, ni vema ukawa jasiri wa maamuzi yatayokufikisha kwenye mafanikio.
Pia wapo watu wanaokuwa thabiti katika kufanya maamuzi, lakini pia, kutekeleza inakuwa shida. “Ni jambo moja kuwa thabiti kufanya maamuzi, lakini ni jambo Jingine kutendea kazi.”
Unapothubutu kufanya jambo lolote ambalo unaona kuwa baadaye litakuletea mafanikio, wewe ni jasiri. Tofauti na hapo unajimaliza mwenyewe, unakuwa mtu ambaye mipango unayopanga inaishia kwenye mikoba.
Yeyote anayewekeza kwenye mradi wowote, anayenunua gari au kufanya uamuzi wa kubadili kazi, anajiwekea mkanganyiko katika maisha yake, lakini mwisho wa yote anavuna furaha na maendeleo kwa kuwa anakuwa amepiga hatua nyingine katika maisha yake, ambayo hakuwahi kuwa nayo.
Kwa upande wa watu ambao hawapendi mabadiliko katika fikra zao kwa jambo lolote, huwa wanakosa kila kitu. Hata kuwa na mafanikio makubwa katika maisha inakuwa ni vigumu.
Kuwa mtu wa kupenda kuthubutu kufanya jambo lolote lenye mafanikio katika maisha.
Unapotaka kusonga mbele, usichukie mawazo ya wengine wenye busara wanaokushauri, japo wapo wengine ambao mara zote hawapendi kuona wenzao wanasonga mbele, jiepushe nao. “ Kuwa na chuki ya kupata maoni kutoka kwa wengine, ni jambo baya ambalo halitakufanya uendelee mbele,” inakupasa uchukue maoni ya kila mmoja na kuyapima. Kamwe usipoteze muda na nguvu zako kutafakari maoni yasiyo na maana.
Mara zote penda kujifunza kutokana na makosa. Kuna msemo mmoja unaosema kuwa, kama umekosea ni vema kukiri kosa lako. Wala usichukie unapoambiwa kuwa umekosea, jifunze kutokana na makosa yako.
Kila tatizo lina utatuzi wake. Kwani hakuna jambo lolote katika sura ya dunia ambalo halina utatuzi. Kila tatizo linalojulikana kwa mwanadamu linapatiwa ufumbuzi.
Japo wakati mwingine tatizo lako linaweza kuonekana ni la kipekee, jua kuwa wengine wameshakabiliana nalo na kulitafutia ufumbuzi.
Matatizo yote yanayompata mwanadamu, ufumbuzi wake unapatikana, kwani kila tatizo lina mlango wake wa kutokea.
Acha kufikiria matatizo unayokutana nayo, hata kama ni mazito kiasi gani, kadiri unavyoruhusu akili yako kufikiria matatizo yanayokukabili ndivyo yanavyozaliwa mengine ambayo hayakuwepo.
Jaribu kupata ufumbuzi wa kila tatizo lililopo mbele yako ili uweze kusonga mbele.
Jipe nafasi ya kufikiri, jipe nafasi hiyo pale unapokuwa na jambo zito linalokutatiza. “Jipe nafasi ya kutulia nyumbani kwako, unapokuwa umekaa kwenye kiti chako, wakati huo utakuwa unapata ufumbuzi wa tatizo linalokukabili.” Wakati huo ni vizuri ukawa na furaha na ushindi wa majibu ya matatizo yanayokukabili.
Ondoa hofu, kwa kuwa mara zote ndiyo inayoharibu uwezo wako wa kuwa na maamuzi ya busara. Kwani hofu inatokana na uamuzi mbaya wa matatizo yako. “Hofu ni adui mkubwa wa matatizo yako.” Inafikia hatua watu wengine huogopa kifo, kutokana na hofu waliyonayo.
Mara nyingine hofu inatokea kwa sababu ya kutokujua ukweli wa jambo, usipoteze nguvu zako kufikiria kitu ambacho haukijui.

Categories:

Leave a Reply