UTAKUWA na tofauti gani katika maisha yako endapo utakuwa mtu wa kujiamini? Ni nini zaidi utakachokipata? Hilo ni swali ambalo sote tunaweza kujiuliza.
Ni ukweli usiopingika, kwamba hali ya kujiamini inasitawisha maisha yako. Hivyo unapokuwa na afya nzuri inakufanya ufikie malengo yako kwa urahisi zaidi.
Unapojiamini katika maisha yako na shughuli zako za kila siku, utaweza kuwasaidia na wengine ambao unawasiliana nao katika maeneo mbalimbali iwe ni nyumbani au kazini. Vile vile endapo unakutana na mambo ya kustaajabisha, ya kushtusha au ya mshangao huna haja ya kuogopa, kwa kuwa tayari umeshajijengea hali ya kujiamini, utaikabili hali hiyo kwa urahisi.
Ni vizuri kujijengea hali ya kujiamini katika maisha yako kwani watu wote walio na hali hiyo wamekuwa na viwango vya tofauti ambavyo kila moja anavifurahia. Kumbuka kuwa hali ya kujiamini na kuwa jasiri, ni muhimu sana katika kila hatua ya maisha yetu, hivyo watu wengi wanajitahidi kuitafuta.
Kwa mtazamo mwingine watu waliokosa hali ya kujiamini inakuwa ni vigumu kwao kupata mafanikio. Kwa upande mwingine, unaweza kushawishika na mtu anayezungumza kwa ufasaha, anayejibu maswali yake kwa kujiamini na anayekuwa tayari kukubali kwamba jambo fulani halifahamu.
Mtu huyo ni rahisi kujifunza jambo jipya ambalo litamwongezea mafanikio zaidi katika maisha yake kwa kuwa yuko tayari. Watu wanaojiamini huambukiza hali hiyo kwa wengine. Hadhira anayokutana nayo, wanachama wenzake, bosi wake, wateja wake na rafiki zake.
Kupata ujasiri wa wengine ni njia mojawapo ambayo mtu anayejiamini huitafuta kwa ajili ya kupata mafanikio zaidi. Habari njema ni kwamba hali hiyo unaweza kujifunza na kuijenga katika maisha yako.
Na endapo unafanya kazi kwa kujiamini au kuwajengea ujasiri watu wanaokuzunguka, unakuwa umefanya jambo jema. Mambo mengine yote yanakuwa sawa kutokana na kujiamini kwako, na yeyote anayejiamini huwa na mafanikio katika maisha yake tofauti na yule mtu ambaye hajiamini. Kiwango chako cha kujiamini kinaweza kuonekana katika njia nyingi. Mfano kutokana na tabia yako, lugha yako, jinsi unavyoongea, kile unachozungumza na mambo mengine mbalimbali. Unawezaje kujijengea hali ya kujiamini?
Ni kwa kufanya kazi ya kutoa ushauri katika mazingira ya kushughulika na watu wa aina mbalimbali, wenye tabia mbalimbali waliovunjika moyo na wanaohitaji msaada zaidi wa kukabiliana na ugumu wa maisha. Unapofanya kazi hiyo ya kutoa ushauri unatakiwa kujua njia sahihi ya kukabiliana na mtu mwenye msongo wa mawazo na kujua ni jinsi gani utaanza mazungumzo naye kutokana na hali aliyokuwa nayo.
“Wakati nilipokuwa naanza kuangalia jinsi ya kuwa na hali yangu mwenyewe ya kujiamini, nilijaribu kuangalia maeneo mbalimbali yatakayonifanya nijijengee uwezo wa kujiamini. Japo kwa mara ya kwanza ilikuwa ni vigumu, lakini ilichukua muda mrefu na niliweza kufanikiwa,” alisema John Robert.
Jambo jingine ambalo linaweza kukusaidia ni kupunguza kumbukumbu za maumivu yatokanayo na mambo yaliyopita katika maisha yako. Hivyo, kama unataka kusonga mbele usikumbuke mambo yaliyopita ambayo yatakurudisha nyuma. Japo ni vizuri kujifunza kutokana na mambo yaliyopita lakini huhitaji kuendelea kuwa na kumbukumbu zinazoumiza.
Ni vyema kama hautafikiria yaliyopita. Hivyo, unaweza ukawa umejifunza wewe mwenyewe mbinu za kujiamini, unapoamua kubadilika na kuwa jasiri, ni kwamba pale unapoanza, utaendelea kukua na kukua.
Unaweza kuendelea kuhisi kwamba pengine unaweza kujiamini zaidi, maisha yanaweza kuwa mazuri kutokana na hali hiyo. Hivyo, mwishoni unafikia ndoto zako kama vile kupata kazi kubwa, kuwa na mahusiano mazuri, kununua nyumba na mambo mengineyo. Unajisikia vizuri wewe mwenyewe na kuwa na furaha kutokana na kile unachokipata. Zipo njia mbalimbali zinazoweza kukufanya ujiamini. Baadhi ya njia hizo zinafanikiwa na nyingine zinashindwa kutokana na mtu mwenyewe.
Wakati mwingine unaweza kujisikia kuwa unahitaji msaada, mtu wa kuongea naye, au kutafuta njia rahisi na kutoa ushauri bila kulipa pesa nyingi. Ni njia ya muda mrefu kuweza kuwa na hali hiyo ya kujiamini lakini inaweza kuwa ni safari nzuri kwa sababu inabadilisha maisha yako. Pia inashangaza kwa sababu unaweza kunufaika zaidi katika kila hatua unavyoongea.
Je, uko tayari kujijengea hali ya kujiamini? Kwanza inakupasa kufanya shughuli mbalimbali ambazo zitakujengea uwezo huo.
“Fanya shughuli za kukujengea ujasiri kila siku na kuwa na mawazo yanayoipanua akili yako,” anasema Mike Bonny. Pia unaweza kujiuliza ni kwa kiasi gani una ujasiri? Hali hiyo inaweza kuwepo kutokana na afya katika akili yako. Kwa mfano, kama unajisikia uchovu muda wote, itakuwa ngumu kuwa jasiri.
Ujasiri katika kufikiri ni jinsi gani mawazo yako yanaweza kuyabadilisha maisha yako. Unapokuwa jasiri katika kufikiri ni sababu ya kuyabadili mawazo tunayoyawaza. Vilevile, ujasiri katika mahusiano mara nyingine unaweza kuona ni kitu cha kukupa changamoto.
Sasa basi, unaweza ukaangalia ulinganisho wa tabia ya kujiamini na ile ya kutojiamini. Ni hatua gani unazoweza kuzichukua kwako binafsi na kwa watu wanaokuzunguka? Unapokuwa mtu wa kujiamini unafanya kile unachofikiri ni sawa, ingawa wengine watakukosoa.
Pia utakuwa tayari kwa lolote ili uweze kupata vitu vizuri. Vile vile unakuwa ni mtu wa kukubali makosa yako na kujifunza. Mtu asiyejiamini anakuwa ameegemea upande wa wengine wanavyofikiri. Unabakia kukaa sehemu moja ukiogopa kushindwa na kukwepa kubahatisha au kuthubutu kufanya jambo fulani. Anakuwa mgumu kukubali kosa.
Kama ulivyoona katika mifano hiyo hapo, hali ya kutojiamini inakuletea uharibifu, bali inakujenga. Jifunze kujiamini, kuwa jasiri katika kila jambo unalolifanya, usitetereke utafanikiwa.

Categories:

Leave a Reply