MSOMAJI wangu, katika mfululizo wa mada, nimedhamiria kukuletea kitu kipya.
Leo tutaangalia jinsi ya kukabiliana na ugonjwa wa kushindwa kufikia malengo.
Kila mmoja tayari ana vifaa vya kutosha katika maabara yake ambayo anaweza kuitumia kwa ajili ya kazi na kujifunza.
Maabara ambayo ina kila kitu kinachokuzunguka katika dunia hii. Ambamo hutapata vikwazo, kwa kuwa kila utakachojifunza utajiona kama wewe ni mtaalamu.
Ukiweza kuitumia vizuri maabara hiyo, itakuwezesha kumaliza matatizo yako ya kifamilia kama vile, kulipia kodi ya nyumba, kulipia ada za shule na mambo mengine yanayofanana na hayo. Hivyo unaweza kuitumia maabara hiyo kwa uhuru zaidi jinsi unavyopenda.
Kwa upande mwingine, unaweza kuwaza jinsi ya kuwa na malengo makubwa katika maisha, kwa kupenda kujifunza kwa wengine waliofanikiwa.
Lakini angalizo lililopo, unatakiwa kujifunza kutoka kwa wengine kwa uangalifu. Pale unapopata jambo linalokufaa lifanyie kazi.
Unapoendelea kujifunza kutoka kwa wengine, utaona kuwa, watu wasiokuwa na mafanikio wanataabika katika akili zao kwa ugonjwa wa kufikiri.
Kila mtu asiyefikia malengo ya mafanikio amekuwa na ugonjwa huo kwa kiwango kikubwa.
Na mara zote mtu mwenye malengo makubwa hupenda kujiuliza ni kwanini hapo alipofikia hajafanikiwa, kwa nini hana kitu fulani au kwanini hawezi kufanya jambo fulani, ili aweze kupiga hatua zaidi ya hapo alipo.
Kama ugonjwa mwingine wowote unavyompata mtu, ugonjwa wa kufikiri unakuwa mbaya sana endapo hautatibiwa vizuri.
Muathirika wa ugonjwa huu, anakuwa akiwaza mambo mengi, kama vile ‘najaribu kufanya jambo hili na lile lakini sipati mafanikio’ na kuendelea kuwaza: “ Je, ni afya mbaya niliyonayo” au ni ukosefu wa elimu? Umri mkubwa? Umri mdogo? Bahati mbaya? Ama kutokuwa na bahati ya maisha? Mke? Ama jinsi nilivyolelewa na familia yangu?”
Hivyo mtu huyo aliyeathirika na ugonjwa huo, asipojigundua ataendelea na hali hiyo katika maisha yake.
Ili kukabiliana na hali hiyo, ni vizuri kujizoeza kuwa na mawazo chanya yenye mafanikio, ambayo ndiyo tiba ya ugonjwa wa kushindwa.
watu wenye ugonjwa wa kushindwa huwa na visingizio mbalimbali kama vile ‘afya yangu siyo nzuri’. Hiyo hufanya kila siku anapopata changamoto ya maisha badala ya kutoka hapo alipo, kuwa na jambo lolote la utetezi fulani.
Anakuwa na afya mbaya katika aina tofauti tofauti, ambacho ndicho kisingizio chake anaposhindwa kufanya jambo linalompatia maendeleo.
Wapo watu wengine wamekuwa wakisingizia wana matatizo ya moyo, na wamekwenda kwa daktari zaidi ya mara nne, na kila wanapokwenda ugonjwa hauonekani.
Kuendelea kueleza kuwa, una ugonjwa wa moyo, mwisho wa siku tatizo hilo litakupata kweli. Kinachotakiwa ni kuishinda hali hiyo na kusonga mbele katika kupata maendeleo yako katika maisha, bila kujali unasumbuliwa na kitu gani.
Sasa basi yapo mambo manne ambayo yanaweza kukupa afya njema na kuondokana na hiyo hali inayokufanya ukate tamaa, ama kufikiria kuwa huwezi kila jambo lililopo mbele yako.
Kwanza usikubali kuizungumzia afya yako. Kadiri unavyozungumzia kuhusu ugonjwa unaokusumbua, hata kama ni wa kawaida, ndivyo utakavyozidi kukusumbua.
Kuzungumzia kuhusu afya yako kama ni mbaya ni kama unaweka mbolea kwenye mbegu zilizopandwa.
Kuzungumzia afya yako ni tabia mbaya. Inachosha wengine. Watu waliofanikiwa wana tabia ya kutokuzungumiza afya zao zinapokuwa mbaya.
Pili usiwe na hofu juu ya afya yako. Fanya kile unachokusudia ili kufikia malengo mazuri.
Tatu, jione kuwa afya yako ni njema haina kasoro. Na pia endelea kujikumbusha kuwa, maisha yapo kwa ajili ya kuyafurahia. Usipoteze. Wala usiishi kwa kufikiri juu ya kulazwa hospitali.
Vile vile usipende kuchunguza kwa nini mipango unayoipanga haifanikiwi, bali ichekeche akili yako kuelekea njia ya mafanikio.

Categories:

Leave a Reply