Tunapozungumzia uwezo wa kujitegemea na kujisimamia mwenyewe tunalenga ule uwezo wa kufanya mambo yako wewe mwenyewe. Namaanisha pia uwezo wa kufanya kwanza kile kinachokuhusu na unachokiweza na ndipo baadae waweza kuomba msaada iwapo inalazimu badala ya kuanza kuomba usaidiwe kabla ya kujaribu wenyewe. Uwezo wa kujitegemea ni muhimu sana katika maendeleo ya mtu binafsi na wengi wamejikuta wanashindwa kupiga hatua maishani, wala kufanya maamuzi yeyote ya muhimu na yatakayoweza kubadilisha maisha yao kwa sababu tu hawawezi kujitegemea kimawazo, kifikra na kimsimamo. Wengi wamekuwa wakiburuzwa tu na watu wengine au na wakubwa wao wa kazi au hata ndugu zao au wazazi wao pasipo wao kuonyesha misimamo au ujasiri walionao. Yamkini unatamani moyoni mwako kufanya au kupata kitu fulani unachokitamani lakini unabaki kuumia sana moyoni maana ukweli ni kwamba wewe binafsi huwezi kukifanya au kukisema hicho unachokitamani bali unabaki kufanya au kusema vile ambavyo wengine wamekuamulia.


Mfululizo wa mada hii utakuwezesha kujijengea uwezo wa kuwa thabiti katika kufanya kile ambacho ulikuwa huwezi kufanya hususan katika kujisimamia na kujitegemea mwenyewe. Labda nitoe mifano michache;
Wako wanandoa ambao mmoja wao hawezi kamwe kujisimamia na kujitegemea kifikra au hata kimaamuzi, mchakato wa kufanya maamuzi yeyote hata yale rahisi unakuwa mgumu sana. Tabu kubwa hutokea pale Mungu anapomchukua mmoja wao.
Wako watu waliooana lakini mmoja wao bado nguvu ya maamuzi yake iko kwa wazazi wake au mzazi mmoja wa upande wake, labda mume hawezi kuamua kitu chochote hadi amsikilize mama yake mzazi, ili ni tatizo kubwa. Au kila mume anachofanya anaambiwa na na kuelekezwa baba yake mzazi. Kwa upande mwingine wako wanawake pia ambao maamuzi ya familia zao hayawezi kufanyika mpaka yaafikiwe au kusahihishwa na mama mzazi wa mwanamke, hapo iko shida kubwa pia. Tofauti au kinyume na kujitegemea ni kuwa tegemezi. Utegemezi ni hali ambayo haifurahishi moyo hatasiku moja na huzuia au kudumaza maendeleo ya mtu.

Tuangalie faida za kujitegemea na kujisimamia mwenyewe.
Ø Utaweza kuvijua vitu au mambo vizuri au bayana zaidi pale utakapo yatafuta wewe mwenyewe na sio kwa kusaidiwa.
Ø Ujasiri wako hukua pale unapojitegemea kimawazo. Ukiwa unauliza kila kitu kwa wenzako, ujasiri wako huathiriwa kwa kiwango kikubwa.
Ø Kwa kujitegemea tunaokoa muda. Unapowategemea wengine sana, unapoteza muda kila wakati kuwatafuta na kuwasubiria ili wakusaidie.
Ø Utaweza kufanya mambo kwa uangalifu mkubwa ukijua kuwa wewe peke yako ndiyo mwajibikaji wa matokeo. Kwa hiyo utaweza kufanya vitu vilivyo vya ubora zaidi.

Tuone pia hasara za kutokujitegemea au kuwa tegemezi kifikra na kiutendaji:
Ø Kutojitegemea mwenyewe sio tu kunakunyima faida zilizotajwa hapo awali bali kunakufanya uishi maisha yasiyo na nguvu (powerless life) na maisha ya kushindwa. Maisha haya baadhi ya wanasaikolojia wameyaita. Ni maisha ya uathirika, Maisha ya kujihatarisha, Maisha ya kuidhinishiwa na Maisha ya kujilaumu.
Uhalisi wa mawazo ya wanasaikolojia hawa umesimama kwenye ukweli kwamba yeyote mwenye tabia tegemezi huwa na fikra au mawazo yafuatayo.

·        Huwa na tabia ya kuwaza kama vile anatarajia kuhatarishwa na kitu fulani na kwa hiyo hubaki kulaumu ile hali ya kufikirika ya ile hatari (hulaumu wasichokiona kama vile kimeshatokea).
·        Hufikiri kwamba kusaidiwa ni haki yao na sio kama zawadi tu, fikra hizi huwadhoofisha na taratibu  huleta matatizo makubwa hususani mmoja anapokuwa kwenye mahusiano kama vile uchumba au hata ndoa.
·        Hufikiri kwamba maisha yake yako hatarini na wengine ndio wanaoweza kumsaidia aondokane na hatari hizo mawazo haya humfanya mtu huyu kujiona mtazamaji tu wakati wengine ndio watendaji.

Watu au mtu mwenye mawazo kama haya anafananishwa na yule ambaye kwa kuhofia ajali za barabarani humkabidhi mtu mwingine gari ili amwendeshe, hata kama ujuzi wa huyo aliyepewapewa kundesha gari ni mdogo.

Watu wajinsi hii au wenyetabia hii huwalaumu na kuwashutumu wengine badala ya kuchukua majukumu ya kuyaendesha maisha yao wenyewe. Tabia ya kulaumu wengine kama wao ndio chanzo cha matatizo yanayotokea kwetu inaathari kubwa sana kimafanikio. Mfano; Kwa kuwalaumu wengine kwa yale yanayotokea kwetu inapunguza hamu ya kujibidisha na kushuhulikia mizizi ya matatizo yetu.

Kuwalaumu wengine kila siku hutushawishi tuamini kuwa sisi ndio wenye matatizo, kwa kuwalaumu wengine kila mara utajiona wewe ndio muathirika na kwamba wao ndio washindi na wanyanyasaji wako. Kwa hali hii taratibu utaanza kujiona uliyemnyonge, dhaifu na wakushindwa na wengine. Ukweli ni kwamba wewe sio mnyonge na wakushindwa, bali tatizo ni utegemezi ulionao kwa wengine.

Nini kifanyike ili kukuza uwezo wetu wa kujitegemea na kujisimamia wenyewe. Zifuatazo ni njia rahisi na zenye ufanisi katika kukuwezesha kukuza uwezo wako wa kujitegemea na kusimama kwa miguu yako.

1. Miliki hisia zao. (Own your feelings)
Hii inamaanisha kwamba inakubidi ukubali na kuamini kuwa wewe ndiye unayeweza kufanya ujihisi vizuri au vibaya hususani pale ambapo mtu fulani amefanya kitu kwako. Mfano; mtu anapofanya kitu au kusema kitu ambacho kinakusumbua hutakiwi kutumia sentensi kama “unanifanya nijihisi vibaya” au “usinifanye nikasirike” bali unatakiwa kusema “Najihisi nimekasirika au “unanitia hasira”.

Pia usiseme “Ulichokisema kimeniudhi sana” badala yake waweza kusema “nimekasirishwa sana na ulichokisema” sentensi hizi “umenifanya nijihisi” na “ninajihisi” zaweza kuonekana zinafanana lakini zinautofauti mkubwa. Katika sentensi ya kwanza unawapa wengine au mtu mwingine uwezo wa kukuudhi, lakini sentensi ya pili inaonyesha umiliki  wako wa kule kujihisi vile unavyojihisi. Iko tofauti ya kusema “umenifanya nijisikie raha” na kusema “ninajisikia raha sana”.
Kwa kutumia sentensi ya kwanza, unajiweka chini ya milki na utawala wa yule anayekusababishia furaha au hasira wakati kwa kutumia sentensi ya pili unamiliki uwezo wa kujipa raha hiyo wewe mwenyewe.

2. Zikubali hisia zako (Accept your feelings)
Ni vema kukubali ukweli kwamba sisi wenyewe ndio tunaojisababishia kuhisi vizuri au vibaya kwa yale ambayo tunajiambia wenyewe, na kwa hiyo basi hatuna budi kukubali kubeba majukumu ya hisia zetu wenyewe. Pia kuwa huru kujiambia au kujinongonezea kitu upendacho mwenyewe ingawa unahitaji kukubali matokeo ya vile utakayojihisi.

Mfano; Umempoteza mtu unayemjali sana na kumtegemea maishani. Waweza kujiambia kuwa “maisha hayana budi kuendelea, nitajipa moyo”
Lakini pia waweza kujiambia; “Basi tena, sintakuwa na mbele wala nyuma, maisha yameshaharibika’ sentensi hizi zote mbili zitakuwa  na matokeo tofauti ndani  yako, ni jukumu lako kuzikubali hisia zako na kuyakubali matokeo yake pia.

3. Fanya kile unachotakiwa  kufanya (Do your assignment)
Wakati wowote unapokuwa na kazi au jukumu la kufanya mfano. Kazi uliyopewa na mwalimu, bosi wako, mwalimu wako wa dini, mzazi wako nk. ifanye akazi hiyo ukijua unaelewa kila kitu kinavyotakiwa kufanyika. Hata kama kwa bahati mbaya unakuja kuonekana umekosea kidogo mwishoni, lakini umeifanya kwa juhudi na maarifa yako mwenyewe. Baadaye waweza sasa kuhitaji maelekezo kutoka kwa wengine nahii itakuwezesha kuwa na uhakika na kile ulichokifanya zaidi ya kutegemea majibu au mwongozo wa wengine kuanzia mwanzoni kabisa.

4. Tafuta kupata taarifa kutoka kwenye vyanzo halisi (Go to the Source)
Wakati wowote  tafuta kufahamu mambo au kupata taarifa yoyote kutoka chanzo halali na chakuaminika, zaidi tu ya kuambiwa na watu ambao hata wao wako kwenye kujifunza kama wewe. Kwa nini utegemee na kusimamia taarifa uliyopewa na aliyesoma gazeti, kwani wewe huwezi kulitafuta ulisome mwenyewe? Kuna watu ambao katika kila wasemacho wakiulizwa wamesikia wapi, husema fulani alisema, hamna hata kimoja walichofanya jitihada za kukitafuta wenyewe, au kushuhudia wenyewe.

Kuna waandishi wa habari ambao huandika habari walizoambiwa na waandishi wenzao waliomsikiliza mhusika akizungumza. Habari za waandishi hawa wawili zitatofautiana, kwa sababu ya ukweli kuwa mmoja amendika alichokisikia kwenye kutoka kwenye chanzo na mwingine ameandika alichokisikia kutoka kwa aliyesikia.

Wataalamu wa mawasiliano wanathibitisha kwamba, kwa kadiri taarifa au habari inapopita kwa watu wengi  kutokea kwenye chanzo husika ndivyo inavyozidi kupotoshwa ule uhalisia wake na mwisho wasiku, wale waliopata habari hiyo baadae sana hupata taarifa yatofauti kabisa, na hata wanapoisema hukosa ujasiri maana hawana uhakika nayo. Kwa tabia ya kupenda kwenda kwenye vyanzo halisi tunaepuka kupotoshwa na wengine na tunajijengea ujasiri katika yale tunayoyafanya au kuyaongea.



5. Epuka kutafuta uhakika toka kwa wengine kila mara
Kila wakati jaribu kufanya kwanza kile unachokiamini. Epuka kuuliza uliza juu ya vitu ambavyo tayari unauhakika navyo, kisa tu unataka walau mtu mwingine akuhakikishie au kukuthibitishia kuwa unachokiamini ni kweli.
Mfano; kama wewe ni mgeni wa mkoa unaouendea wa Dodoma na mabango unayoyaona yanakuonyesha jina la eneo au mji wa Dodoma, hakuna haja ya kuuliza mtu mwingine “eti ndio tumeshafika Dodoma’. Wakati kila bango na ishara inakuonyesha kuwa tayari uko Dodoma. Tofauti na swali la kwanza, waweza kubadili na kutumia sentensi na kusema “Angalia Dodoma inavyopendeza” kama umekosea chochote, mtu huyu wapili ataweza kukusahihisha.

6. Epuka maelezo yenye viulizo vya maswali (Avoid Questions tags)
Ingawa maelezo yenye viulizo vya maswali ni muhimu katika mawasiliano, lakini ikiwa nia ni kujenga uwezo wa kujitegemea na kujisimamia maswali haya sio mazuri, hususani pale ambapo  nia ni kumfanya mwingine kutuhakikishia au kututhibitishia kile talichokiongea. Njia rahisi ni kujiuliza wewe mwenyewe kuwa ungejisikiaje ikiwa huyu mwezako uliyemuliza asingekubaliana na kile ulichokisema?
Mfano; Epuka kusema “Nimependeza! si ndiyo? Badala yake sema “nimepandeza”. Sentensi ya kwanza yenye swali na “si ndiyo?” humpa uwezo na mamlaka aliyeulizwa kukupa uhakika wa kupendeza kwako au kukukatisha tama kuwa kujapendeza, bali sentensi ya pili isiyo na swali la
“si ndiyo?”kukupa umiliki wewe mwenyewe, pasipo kumtegemea yeyote kuthibitisha juu ya kupendeza kwako.

7. Epuka mijadala yenye mabishano (Avoid heated discussion)
Badala  ya kujiingiza katika mijadala yenye misuguano ili tu kuwashawishi wengine waone unachoongea ni cha ukweli jaribu kukaa kimya na kwa utaratibu na ufupi ukiseme unachokisema ukikiaminikuwa ni cha kweli.
Mijadala yenye mabishano na mivutano huonyesha kuwa hatuna uhakika na kile tunachokiongea na kwa hiyo tunakuwa na hofu pale ambapo wengine hawatuungi mkono.

Kibaya kingine kinachoweza kukutokea unapojiingiza kwenye mijadala yenye misunguano ni kwamba unabaki kuwa kichekesho kwa wale wanaokusikiliza na kukuangalia, mara unajigundua kuwa kila unapoanza kuongea wengine wanacheka, utajiumiza kichwa bure, na kumuumiza kichwa yule mnayebishana naye. Tatizo baadae utajisikia kuhukumiwa na kujilaumu, wakati mjadala wowote wenye kujenga kamwe hauna majuto.

8. Heshimu mawazo ya wengine (Respect others issues)
Kumbuka kwamba watu hutoa mawazo yao wakiamini kuwa vile wanavyovisema ni vya kweli. Yamkini wanayaamini mawazo yao maana wana uzoefu wa muda katika vile wavavyovisema na ndiyo maana wanathubutu kusema hivyo wanavyovisema, watu hawa wanahakika kuwa wayasemayo ni kweli sawa sawa na vile wewe unavyoamini kwamba unayoyasema ni kweli.

Ili kubadili mtazamo huu wa mtu yahitaji uwezo wa ushawishi na kujadiliana kwa upendo. Mtu mwenye busara daima huanza kwa kuheshimu mawazo ya wenzake na siyo kuyapinga na taratibu baada ya kuyaheshimu, huanza kuonyesha ubora wa yale aliyonayo na mapungufu yaliyopo kwa yale wengine waliyonayo. Kamwe usianze kwa kuponda, kulaumu au kukejeli, kwasababu kwa kufanya hivyo yawezekana ukafunga milango hata kwa mawazo yako kutopokelewa tena.

9. Jenga tabia ya kutembea hatua ya zaidi (Learn the habit of going a step further)
Hii ni tabia ya kuweza kufanya zaidi ya ulichoambiwa au ulichoagizwa pasipo kutegemea au kutarajia malipo au upendeleo tofauti. Kama utakuwa na tabia hii kamwe hutahitaji mtu wa kukusimamia ili umalize kazi yako. Watu wenye tabia hii pekee ndio wenye uwezo wakuwa mabosi juu ya kazi zao wenyewe. “bosi wako anakuwa ni wewe mwenyewe”. Ziko aina mbili mbaya sana za watu kinyume na hii niliyoitaja hapa juu. Wako wale wasioweza kufanya lile wanalotarajiwa kulifanya. Na pia wako wale ambao hufanya tu lile walilotarajiwa kulifanya. Kamwe wewe usiwe kati ya hawa.

10. Kuwa mgunduzi (Be innovative)
Huu ni uwezo wa kutumia njia mbalimbali, mawazo mbali mbali na jitihada mbalimbali ili kushuhulikia  changamtoto za kila siku maishani.
Ili kuwa mgunduzi yahitaji mtu mwenye mitazamo au tabia za aina mbili.
(a)  Kwanza yakupasa uitazame elimu tunayoipata mashuleni kama nyenzo ya kutusaidia kuyashuhulikia matatizo ya maisha. Hii ina maana, utatumia yale uliyoyapata au kufundishwa shuleni au chuoni kuyakusianisha na utatuzi wa changamoto za maishani na kamwe hautamhitaji tena mwalimu akueleze jinsi ya kufanya kila kitu.
(b)  Aina nyingine ya tabia ni ile ya kuweza kuziamini njia na mbinu unazozigundua wewe mwenyewe. Unapogundua au kuwaza kitu na ukaona kinauwezo wa kutatua changamoto fulani kimaisha basi endelea kukitumia au kuzitumia mbinu hizo mradi tu mbinu hizo ziwe zenye maadili. Kama wewe ni mtu usiyeweza kujitegemea na kujisimamia mwenyewe kamwe hutoziamini mbinu ulizozigundua  hata kama mbinu hizo zinaonekana kufanya kazi, kwa kuwa wewe mwenyewe hujiamini. Kwa kuwa mgunduzi kutakuongezea uwezo wa kujitegemea na kujisimamia.

Categories:

Leave a Reply