Na Charles Msuluzya Nazi
17. Mazao ya chakula
Biashara ya kununua na kuuza mazao ya chakula ni biashara nzuri ambayo
ina faida kubwa na pia soko lake ni la uhakika kwa sababu kila mtu
anahitaji chakula. Bei za mazao huwa zinabadilika mara kwa mara
kufuatana na msimu. Kwa mfano; wakati wa mavuno mazao huwa na bei ndogo
na kupatikana kwa wingi ubunifu ni kuhamisha kutoka huko kwenye wingi na
kuyauza kwenye uhaba kwa faida kubwa. Au unaweza kununua kwa wingi na
kuhifadhi hadi msimu wa uhaba nawe ukauza kwa faida kubwa. Biashara hii
inahitaji uwe na mtaji pia na maghala ya kutunzia mazao hayo. Unapaswa
kujifunza mbinu za kuhifadhi mazao kama vile kuweka dawa za kuua wadudu
ili mazao yasiharibike. Unaweza ukaamua kuwa mkulima wa mazao, kuyalima
na kuyauza au kununua mazao na kuyauza. Ni muhimu kufanya utafiti wa
soko la mazao yako kabla ya kufanya biashara hii ili usije ukashindwa
kuyauza.
18. Huduma za kitaalamu.
Biashara ya kutoa huduma za kitaalamu ni nzuri sana na ina mapato
mazuri, inaweza kuleta utajiri na maisha bora. Ili ufanye biashara hii
unapaswa kwanza kusomea taaluma husika kwa kiwango kinachohitajika na
wahitaji au masoko. Taaluma ambazo zina malipo mazuri ni ufundi, ualimu,
uanasheria, udaktari ufamasia, uhasibu na ufundi wa vifaa vya
elektroniki. Unaweza kuanza kwa kuajiriwa kwenye ofisi inayotoa huduma
ya fani yako ili upate uzoefu na siri ya biashara hiyo. Kisha tafuta
kuanza taratibu kufanya kazi zako binafsi. Ukiona biashara yako inaenda
vizuri acha kazi na uende kufanya biashara yako kwa juhudi na maarifa
yako yote na utafanikiwa.
19. Magari ya usafirishaji.
Biashara ya usafirishaji ni biashara pana sana ambayo inajumuisha magari
ya abiria na magari ya mizigo. Ni biashara yenye faida sana,
inayohitaji mtaji mkubwa na usimamizi wa hali ya juu ili kudhibiti wizi
wa mapato. Kwa kuwa biashara hii ni pana kila aina ya biashara
tutaizungumzia hapa nchini.
(i) Kusafirisha abiria
Biashara hii ni nzuri na inayo mapato mazuri ya uhakika. Ili uweze
kufanikiwa katika biashara hii unatakiwa ununue gari ambalo ni zima.
Usimamie kwa karibu na kudhibiti mapato ili yasiibiwe. Gari linatakiwa
lifanyiwe ukarabati mara kwa mara ili liwe katika hali nzuri ya kufanya
kazi. Uweke akiba nusu ya mapato ili kukabiliana na dharura ya
matengenezo makubwa. Niliwahi kuzungumza na aliyekuwa mmiliki mmoja wa
magari ya kusafirishia abiria kuhusu suala hili ambapo alisimulia mkasa
uliomkuta. Yeye alikuwa analetewa mapato yake katika kumbi za starehe na
kutumia hizo fedha, kunywea pombe. Alikuwa haweki akiba. Siku moja gari
liliharibika na lilihitaji matengenezo ya Tshs 900,000/=. Mmliki huyo
wa magari ya kusafirishia abiria alikuwa hana fedha hivyo aliamua kuuza
gari. Matatizo ya aina hii ya biashara ni kuwapo watu wengi wanaotegemea
kuchota mapato hayo nao ni dereva, kondakta, mawakala na kadhalika. Pia
kuna udanganyifu mwingi unaofanywa na dereva na kondakta kwa kusingizia
kuwa gari limeharibika au limekamatwa na askari wa usalama barabarani
wakati siyo kweli ili mapato wayaibe. Pia kuna wizi wa mafuta na vipuri.
Ili kukabiliana na matatizo haya unaweza kumwekea kiwango maalum cha
mapato anayopaswa kuwasilisha na dereva na kondakta. Kwa mfano, kwa gari
la uwezo wa kubeba abiria 18 kiasi cha mapato ni Tshs 25,000/= kwa siku
na gari la abiria 26 mapato ni Tshs 40,000/= kwa siku. Pia unapaswa
kufuatilia nyendo za wafanyakazi hao. Unaweza kuingia mikataba na
makampuni ya kusafirisha wafanyakazi au wanafunzi ili upate mapato ya
uhakika pia.
(ii) Magari ya kukodi
Biashara ya taxi ni nzuri na ina faida kubwa. Tatizo lake ni gumu
kudhibiti kwani soko la abiria halina uhakika kama magari ya abiria ni
rahisi dereva kukuambia kwamba hajapata abiria siku nzima. Pia kuna wizi
wa mafuta na udanganyifu kwa kisingizio cha kuharibika gari. Katika
biashara hii unatakiwa ununue gari zima, ulifanyie ukarabati mara kwa
mara ili liwe katika hali nzuri ya kufanya kazi.Umfuatilie dereva wako
katika nyendo zake ili uwe karibu nae kwa msaada atakaotaka na
urejeshaji mzuri wa mapato. Unaweza kudhibiti mapato kwa kumwekea dereva
wa taxi kiwango cha mapato cha kuwakilisha kwa siku ambazo ni Tshs
10,000/= Unaweza kuingia mkataba wa kukodisha kwenye makampuni
kusafirishia watalii au wageni na kupata mapato ya uhakika.
(iii) Magari makubwa ya abiria
Biashara hii ni nzuri. Inahitaji mtaji mkubwa kwani gari moja, linaweza
kununuliwa hadi kwa Tshs 100,000,000/= Inahitaji uthibiti wa mapato kwa
hali ya juu kwani kuna watu wengi ambao wanategemea kuchota mapato ya
gari kama vile dereva, kondakta, mawakala, wahudumu wa magereji na
kadhalika. Kuna udanganyifu mwingi unaofanywa na wafanyakazi li
wakuibie, kama vile kusafirisha abiria wa njiani na mizigo. Bila
kuonyesha ankara na wafanyakazi kuchukua fedha za nauli bila
kuziwasilisha. Pia kuna wizi wa mafuta, kusingizia gari kuharibika
wakati ni zima au kusingizia kukosa abiria ili wachukue fedha za nauli.
Ili kukabiliana na matatizo hayo unapaswa: kununua gari zima na
kulifanyia ukarabati mara kwa mara ili gari liwe katika hali nzuri ya
kufanya kazi. Simamia gari lako kuhakikisha linajaza abiria kabla ya
safari. Unaweza kuweka wakaguzi na kufanya ukaguzi wa kushitukiza njiani
ili kubaini udanganyifu wa kupakia abiria wa njiani na mzigo bila
kuwakatia tiketi. Weka akiba nusu ya mapato kukabiliana na gharama za
matengenezo makubwa au dharura. Ajiri wafanyakazi waadilifu na pia
uwalipe vizuri na uwape motisha. Ii kujipatia mapato ya uhakika, kama
una magari mengi unaweza kuingia mkataba na watu binafsi au makampuni
kusafirisha wafanyakazi au wanafunzi.
(iv) Magari ya mizigo
Biashara hii ni nzuri. Ina faida kubwa pia. Wingi wa mapato unategemea
na ukubwa wa gari. Ili ufanikiwe katika biashara hii, unapaswa kununua
gari zima kulifanyia ukarabati kila mara ili kuliweka katika hali nzuri
ya kufanya kazi. Pia unatakiwa kutafuta wateja wa kukodisha gari lako
kwa kungia mkataba na wafanyabishara ili kuwasafirishia mizigoyao.
Unaweza kuliegesha gari lako sehemu ambayo kuna wateja wanaohitaji
kusafirisha mizigo, kama vile sokoni, kwenye maduka ya jumla au
viwandani. Matatizo ya biashara hii ni kuwapo kwa watu wengi
wanaotegemea mapato ya gari lako ambao ni dereva, utingo, mawakala na
kadhalika. Pia kuna udanganyifu unaofanywa na wafanyakazi kama vile,
kubeba mizigo bila kuwasilisha fedha, wizi wa mafuta, kusingizia gari
kuharibika au kukamatwa askari wa usalama wa barabara wakati sio kweli
ili wakuibie fedha za usafirishaji wa mizigo. Ili kukabiliana na tatizo
hili ajiri wafanyakazi waaminifu, uwape motisha na kuwalipa mshahara
mzuri. Unapaswa pia kufuatilia nyendo za wafanyakazi wako.Tafuta pia
wafanyabishara wakubwa au mashirika kusafirisha mizigo yao ili upate
mapato ya uhakika.
CHARLES MSULUZYA NAZI
Mwandishi wa makala hii ni mshauri wa biashara na mtunzi wa kitabu cha
Mbinu za biashara na maarifa ya kupata pesa na utajiri. Kwa mawasiliano
piga simu namba 0755394701 barua pepe cnazi2002@yahoo.com http://www.squidoo.com/
CHARLES NAZI
Senior Internal Auditor-General Accounting
TANESCO LTD | Umeme Park-Ubungo
P.O.BOX 9024 | Dar es salaam
Mobile: 255755394701 | land line255222451230
Website: www.tanesco.co.tz
We light up your life.
Categories: