Wengi Wetu tunaishi katika mazingira ambayo yanaathiri sana amani yetu ya moyoni. Yamkini tunaonekana tunafuraha, tunacheka tunahusiana vema na wanaotuzunguka lakini ukweli ni kwamba ndani yetu hatuko sawa. Wengi tunawaona wana maisha mazuri sana kwa jinsi ya nje, wana majumba mazuri ya kuishi, wana magari mazuri ya kutembelea, watoto wazuri na kazi nzuri pia na tukiwaangalia tunadhani wanafuraha sana ndani yao lakini nimepata bahati ya kuzungumza na wengi wa aina hii na kugundua kuwa hawakuwa na furaha ya maisha yao kama wengine walivyofikiri. Viko vitu vingi vinavyoweza kuiathiri amani ya moyoni mwako, kwa mfano; hali mbaya ya mahusiano baina yako na umpendaye, matatizo ya tabia za watoto wako, matatizo ya kazini kwako, kushindwa kufikia malengo binafsi, historia yako binafsi, maumivu ya moyo, mambo ya ndugu na mengine mengi.
Dhumuni
langu katika makala hii ni kujaribu kuzibua kanuni chache za kusaidia
kuishulikia hali hii ili uweze kupona katika tatizo hili.
1. Jitahidi kutokuingilia mambo ya wengine, labda tu uruhusiwe na mhusika
Wengi
tumejikuta katika matatizo sababu tu ya kuingilia mambo yasiyokuwa
yetu, tunafanya hivyo sababu mara nyingine tunafikiri tunavyojua sisi
ndio sawa, na mtazamo wetu ndio ukosahihi zaidi, na yeyote
asiyeafikiana na mtazamo wetu anastahili kupingwa. Lazima tutambue
kwamba Mungu amemuumba kila mmoja wetu tofauti. Hakuna watu wawili
watakao waza au kutenda sawa sawa. Jali yaliyo yako kwanza na utailinda
amani ya moyo wako (mind your own business).
2. Jifunze kusamehe na kusahau
Hii
ni nguzo na msaada mkubwa katika kutafuta amani ya moyoni. Mara nyingi
tunaweka hisia za maumivu moyoni dhidi ya mtu aliyetuumiza au kutuudhi,
taratibu tunaumba na kulea chuki kali moyoni. Matokeo yake wengine
wanakosa usingizi, wanapata vidonda vya tumbo, wengine shinikizo la damu
(BP) n.k. Chuki au maumivu haya ya moyo yalifanywa mara moja, lakini
matokeo yake yanaeendelea kuharibu maisha na afya kwa muda mrefu kwa
sababu tu ya wewe kuikumbuka chuki au uchungu. Achana na tabia hii
mbaya. Maisha ni mafupi sana hustahili kuyaweka katika matatizo yote
haya. Samehe, sahau na tembea mbele. Upendo wakati wote huchanua
katika tendo la kutoa na kusamehe (love flourishes in giving and
forgiving )
3. Kamwe usijitutumue kutafuta umaarufu, kujulikana au kutambulika
Fahamu
kuwa ulimwengu huu una wabinafsi wengi sana, mara chache watakusifia
pasipo kuwa na wivu. Wanaweza kukusifia leo kwa sababu unanafasi au
uwezo fulani, lakini subiri utakaposhuka chini. Watasahau kabisa yote
mema uliyofanya na kuanza kutafuta kila chafu na ovu ulilotenda, hata
kama lilitendeka mafichoni. Kwa nini unataka kujiua ukitafuta
kutambulika na kukubalika. Kwamwe kukubali kwao hakulingani na kero
zao. Kero zao zinazidi sana. Jitahidi kufanya majukumu yako kwa nidhamu
ya hali ya juu na moyo wote, ukimwogopa na kumheshimu Mungu na sio
mwanadamu.
4. Usiwe na Wivu
Wote
tunajua jinsi wivu unavyoweza kusumbua amani yetu ya moyoni. Unajua
kabisa kuwa unafanyakazi zaidi ya wenzako ofisini lakini wao wanapata
kupandishwa cheo au faida zingine za kikazi na sio wewe.
Wewe
umeanza biashara miaka tele iliyopita, lakini haujafanikiwa kama
jirani yako ambaye ana mwaka tu katika biashara. Iko mifano tele kama
hii katika maisha ya kila siku. Je ndio inakufanya uwe na wivu?
Hapana, kumbuka kuwa kila maisha ya mtu hutegemezwa na mustakabali wake
utakavyokuwa, ambao ndivyo unavyompeleka yeye hivyo alivyo. Kama
umepangiwa kufikia hatua fulani hakuna atakayeweza kusimamisha. Kama
hujapangiwa hivyo, hakuna atakayeweza kukusaidia kufikia pale pasipo
pako. Hakuna utakachokipata kwa kulaumu wengine kwa bahati zako mbaya.
Wivu hautokupeleka kokote, zaidi utakuondolea amani moyoni mwako.
5. Jifunze kubadilika kutokana na mazingira
Kama
unadhani utaweza kushindana na mazingira na kuyabadilisha, kuna
uwezekano mkubwa kuwa utafeli. Badala yake jifunze kubadilika wewe
kwanza ili kuendana na mazingira yanayokuzunguka, ambayo unadhani yako
kinyume na matakwa yako. Kwa kufanya hivi hata mazingira yaliyoonekana
kuwa magumu taratibu yatabadilika na kuwa ya kuridhisha.
6. Jitahidi kustahimili vile visivyoweza kubadilika (Endure what cannot be cured)
Hii
ni njia bora yakugeuza bahati mbaya kuwa bahati nzuri. Kila siku
tunakutana na matatizo, balaa, magonjwa, hofu na hata ajali ambazo ni
zaidi ya uwezo wetu. Kama hatuwezi kufanya chochote dhidi ya mambo haya
magumu wala hatuwezi kuyabadilisha basi ni vema tujifunze kustahimili,
kukubali na kuchukuliana na hali tukiwa bado wenye tumaini. Jiamini
wakati wote unapoyapitia haya na utaona mbegu ya ujasiri na uvumilivu
inaota ndani yako na taratibu nguvu ya kuendelea mbele itaibuka.
7. Kamwe using’ate zaidi ya unavyoweza kutafuna
Mara
zote kumbuka wazo hili, maranyingi katika maisha haya yenye mahangaiko
tele na kiu ya kufikia malengo makubwa wengi wetu tumejikuta tunachukua
majukumu mengi kuliko uwezo wetu wa kuyatekeleza. Maranyingine
tunafanya hivi kwakuzifurahisha nafsi zetu tu. Fahamu ukomo wa uwezo
wako, kwanini uchukue mzigo ambao utakuzidishia matatizo? Hutoweza
kupata amani moyoni kwa kuongeza mipaka ya majukumu yako ambayo
yanakuzidi. Punguza majukumu na tumia muda mwingi utakaoupata katika
kutafakari jinsi gani utaboresha yale machache unayoyafanya. Tumia pia
muda wako kwa kuongeza ubora wa mahusiano yako na wale wanaokuzunguka
kuanzia familia, marafiki na kwa jinsi hii lazima utahisi amani tele
moyoni na nafsini mwako.
8. Pata muda wa kutafakari mara kwa mara
Kutafakari
hutuliza akili nafsi na kupunguza au kupooza mawazo masumbufu. Hii
ni aina ya juu zaidi ya kutafuta amani ya moyoni na nafsi.
Imechunguzwa kwamba kama utaweza kutumia angalau lisaa kutafakari kila
siku basi utaweza kuendelea kuwa na amani nafsini na moyoni katika masaa
mengine yote yaliyobaki katika siku hiyo. Nafsi na moyo wako
havitaweza kusumbuliwa kwa urahisi tena kama ilivyokuwa awali. Taratibu
utaongeza muda wako wa kutafakari, na matokeo yatabadilika zaidi pia.
Najua unaweza kuwaza kuhusu muda unaopotea hapo, lakini kinyume chake
hii itaongeza ufanisi na kuboresha matokeo ya kila utakacho kifanya,
tena katika muda mfupi.
9. Kamwe usiiache nafsi yako pweke
Kuna
msemo wa kiingereza unaosema “An Idle mind is the devil’s wadshop”,
ukimaanisha kuwa nafsi iliyoachwa pweke pasipo chakufanya wala
chakufikiri ndio karakana ya ibilisi ya kufanya mambo machafu. Wakati
wote iweke nafsi na moyo wako katika kuwaza yaliyobora, yanayojenga na
yakimaendeleo. Amua kuyawaza yale unayoyathamini. Je unathamini pesa
zaidi ya amani ya nafsini mwako? Vitu kama kazi za kijamii, kujitolea,
Ibada, unavithamini kwa kiasi gani? Yamkini vinaweza visiwe na
uthamani wa kifedha lakini vinaweza kukupa utoshelevu wa moyoni kwa
kiasi kikubwa. Hata kama umepumzika, iruhusu nafsi , moyo na akili yako
kufanya vitu vya kiafya kama vile kusoma mambo mazuri, kubadilishana
mawazo, nk.
10. Usipende kujiweka njia panda na usiruhusu majuto
Utapoteza
muda mrefu, masaa, siku wiki na hata miaka kama kila siku unajiuliza
“sijui nifanye nini kati ya haya? Usijiingize katika mijadala isiyo na
mwisho ya nini kifanyike. Najua ni vema kuwa na malengo, lakini
hatuwezi kupanga kwa kikamilifu kwa asilimia 100, maana hatuwezi
kutabiri yaliyombele yetu. Thamini muda wako na tenda yale mambo ambayo
yanaumuhimu na uwezo wa kufanyika.
Haijalishi
kama utashindwa mara ya kwanza, bado utaweza kujifunza kutokana na
kushindwa huko ili ufanikiwe siku nyingine. Kukaa na kuanza kufikiria
kule kushindwa kwako hakutokusaidia chochote. Jifunze kutokana na
makosa yako ila using’ang’ane na makosa yako ya awali. Jifunze
kutokujuta ovyo, yamkini kilichotokea kilipangwa kitokee vile
kilivyotokea kwa makusudi fulani, yanini kulilia maziwa yaliyokwisha
kumwagika?
Kuna
maandishi niliyasoma katika kitabu fulani yakielekeza namna ya maneno
ya kukusaidia kupata amani ya moyo kila siku, wewe pia waweza kuyatumia
maneno haya na yatakusaidia.
Mungu nisaidie kuweza kuleta mabadiliko
katika yale ambayo nina uwezo wa kuyabadilisha.
Ni saidie kuweza kuyakubali yale nisiyoweza kuyabadilisha,
na kuifahamu tofauti iliyopo baina ya haya mawili.
Categories: