Ndugu mdau ngoja leo tujaribu kutumia maandiko kidogo ili tuzidi kujiimarisha kimwili na kiroho ili tuweze kupata mafanikio ya kweli.
Mapungufu humkwaza mwanadamu kufikia ndoto yake katika maisha. Kuna mapungufu mengi naya aina mbalimbali yanayoweza kunifanya nishindwe kabisa kuitekeleza ndoto yangu katika maisha. Kuna mapungufu ya kiasili kama ya kimaumbile, urefu, ufupi, genda nk. tujaribu kumtumia ZAKAYO, alikuwa na mapungufu makubwa mawili. Kwanza alikuwa na mapungufu ya kiasili, alikuwa mfupi. (Lk.18:3). Mtu mfupi akiwa katika mkusanyiko mkubwa wa watu, hana bahati kwani mtu mrefu akisimama mbele yake basi hawezi kuona mbele. Huu ni upungufu, Zakayo hawezi kumuona Yesu kwani watu waliokuwa wamemzunguka Yesu ni wengi na warefu.

Zakayo alikuwa mtoza ushuru mkuu. Mtoza ushuru mkuu wakati wa Yesu alikuwa mtu mwenye uwezo mkubwa sana kifedha, kwani, Warumi waliokuwa wameitawala Israeli wakati huo walitaka walipwe ushuru mbele. Mtoza ushuru mkuu alikuwa ni mtu mwenye mtaji wa kuweza kulipa ushuru wa mji mzima kabla ya kukusanya. Akisha lipa Warumi, yeye hutafuta watu wengine wamsaidie kukusanya ushuru ili arudishe pesa zake na ziada ilikuwa faida yake. Waisraeli waliwachukia sana watoza ushuru kwani walikuwa wanalangua ushuru na hivyo kuwasaidia wakoloni kuwanyonya Waisraeli wenzao. Hili ni pungufu jingine kubwa la kijamii.

Zakayo mtoza ushuru tajiri ana ndoto maishani. Ndoto yake ni kumuona Yesu. Utajiri na mali alizokuwa nazo haumpi amani. “Hata matajiri hulia.” Kuna watu wengi duniani wenye uwezo mkubwa wa kifedha, lakini maisha yao yamejaa utupu na upweke. Mali haziwezi kuijaza furaha ya kweli moyoni. Kama una mali na huna uhusiano mwema na majirani zako, huwezi kuwa na amani. Ukiwa na mali nyingi na nyumbani mwako hakuna amani, vita kila siku huwezi kuwa na amani, ukiwa na mali nyingi na hakuna mtu anayesema jambo lolote zuri kukuhusu huwezi kuwa na amani. Mali isiyomuweka Mungu mbele ni mateso na utupu mtupu. Hii ndiyo maana watu wengi wenye mali nyingi na majina makubwa ambao hawamchi Mungu, wameishia kuishi maisha ya upekwe na hata wengine wamefikiria kujiua. Zakayo alikuwa mmoja wa watu wa kundi hili, ana mali nyingi lakini watu wanamsema vibaya.

Pamoja na kuwa Zakayo anayajua mapungufu yake ya kiasili (ufupi) na ya kijamii (chuki), Zakayo mtu wa jitihada, hakubali mapungufu hayo kuwa kikwazo kwake kumuona Yesu. “Palipo na nia pana njia.” Anaangalia angalia na anauona mkuyu. Zakayo anajua anataka kumuona Yesu na basi mkuyu utampatia nafasi hiyo. Anakwea mkuyuni na hivyo kutimiza ndoto yake maishani. Kukwea mkuyu kwa mtu wa hadhi yake halikuwa jambo la kawaida, ilikuwa aibu kubwa kwani miti hukwewa na watoto na pia ni hatari kwani angeweza kuanguka toka juu ya mkuyu. Hili lingekuwa jambo la aibu kubwa kwa mtu tajiri kama yeye kupanda mkuyuni. Lakini Zakayo si mtu wa kutoa sababu za kushindwa kufanikiwa katika maisha yake. Ni mtu anayeiona nafasi na kutia bidii zote ili afanikiwe. Na tunavyoona Zakayo anafanikiwa kumuona Yesu. Yesu alizituza juhudi za Zakayo kwa kumuita, “Zakayo, shuka upesi, kwa kuwa leo imenipasa kushinda nyumbani mwako.” (Lk. 18:5)

Yesu anamtumia Zakayo kutuonyesha jinsi Mungu anavyozijali juhudi za wale wajitahidio bila kukata tamaa. Kama Zakayo asingejitahidi kutafuta mbinu za kumuona Yesu, hata kwa kupanda mkuyuni, angekufa bila kutimiza ndoto yake maishani.

Watu wengi tunashindwa kutimiza ndoto zetu maishani kwa kuogopa mapungufu tulivyokuwa nayo. Mapungufu tuliyokuwa nayo yanatutia woga. Tunatafuta vijisababu kuhalalisha kutokufanikiwa kwetu. Ndoto ni wito rohoni ambao utamfanya mtu asiwe na raha na amani kama ndoto hiyo haijatizwa. Lakini tunaweza kuizika ndoto yangu kama ninaweza kujisadikisha kuwa nsikuwa na uwezo wa kuitimiza. Zakayo alikuwa na ndoto na alikuwa na mapungufu lakini hakuacha mapungufu yawe vikwazo alitafuta namna ya kuvikwepa vikwazo. Iko njia, iko namna katika maisha ambayo unaweza kutumia kuvikwepa vikwazo vinavyokufanya ushindwe kufanikiwa. Usifurahie sababu ya kutokufanikiwa katika maisha, furahia mafanikio. Mungu anapenda watu wanaotia jitihada katika maisha.

Hakuna kikwazo kisichokuwa na mkuyu. Inabidi tuachane na tabia ya asili ya kutoa lawama na kushindwa kutimiza ndoto zetu katika maisha. Ndoto ni shauri la waliolala, inabidi ukishaota uamke n uanze kuifuata njozi yako. Ndoto ukiamka si ndoto tena bali ni njozi inayompa mtu mwelekeo. Ukiota na ukibakia kulala, itaendelea kuwa ndoto na hakuna siku itakaa ihitimishwe. Itakuwa ndoto ya alinacha ama uzushi mtupu.

Hivyo basi tusipoteze muda mwingi tukisema kama ningekuwa kabila hili, ama lile ningefanikiwa; Kama ningekuwa na uwezo huu ama ule basi mambo yangu yangeenda vizuri; Kama ningekuwa mwanaume ama mwanamke ningefanya hivi ama vile; Kama muda huu, ndio ningekuwa mwanafunzi, ningesoma sana ili niwe na maisha mazuri zaidi. Mwanafunzi naye anasema, ningekuwa na akili kama fulani, ningefanya vizuri; ama ningekuwa shule bora zaidi ningesoma kwa bidii sana. Hizi ndoto za mchana hazitatusaidia. Kitakachotusaidia ni kukubali mapungufu yetu na hapo kuangalia ni kitu gani Mungu ametuwekea karibu kitakachotuwezesha kutimiza ndoto zetu. Kama Zakayo asingekuwa mtu wa jitihada, asingeona kuwa angeweza kupanda mkuyuni na hivyo kuyashinda mapungufu yake.

Sisi pia, inatubidi, kuangalia kwa makini kabisa ni mapugufu gani yanayotufanya tushindwe kutimiza ndoto zetu maishani.(ulevi? Wivu? Tamaa? Hasira? Uwongo? Nk.) Baada ya kuyaona mapungufu hayo, tuangalie kwa makini, tena sana, ni kitu gani Mungu ametuwekea karibu nasi ambacho kitatufanya tuweze kuyashinda mapungufu haya. Ndiyo tumuombe Mungu kwa bidii zote, kwani yeye alikuja ili tuwe na uzima kamili (Jn 10:10) na siyo mapungufu

Maisha hayataki visababu yanataka jitihada na ubunifu. Maisha yanataka kumuamini Mungu anayetuwezesha kufanikiwa katika maisha. Maisha ya kiroho nayo hayataki uzembe. Yanataka nidhamu ambayo hujengwa kwa jitihada nyingi. Kuhudhuria ibada, kupokea sacrament za kanisa na pia kuwa mtu wa maombi bila kutafuta visababu maishani. Utakapo isikia sauti ya Yesu maishani, utapata amani ambayo hujawahi itakuweza kuwa na mtazamo tofauti wa maisha. Tukumbuke kuwa Yesu hakumwambia Zakayo kuwalipa watu aliowadhulumu. Yesu hakumwambia Zakayo atoe nusu ya mali yake kwa masikini. Yesu alipojialika nyumbani kwa Zakayo, Zakayo alipata ahueni na akayaona maisha yake tofauti kabisa, akajua kuwa furaha ya kweli haikuwa katika kujikusanyia mali bali kuwa katika ushika na Mungu ambao hautengi jirani na hasa wenge shida mbalimbali. Mali iletayo furaha na amani ni ili itumikayo kwa ajili ya manufaa ya watu wengi, ni mali itumikayo kuwasaidia watu. Ni mali ambayo watu watakuombea kwa Mungu wakisema, “Mungu ambariki, kwani nimesaidika.” Pamoja na kuwa Zakayo haachi kutoza ushuru, kutoka sasa atatosa ushuru wa haki, atawasaidia masikini na atakuwa na marafiki watakao muachia nafasi katika mkusanyiko wa kumuona Yesu.

Zakayo aliona mti wa mkuyu, wewe pia inakubidi utafute mkuyu wako utakao panda, na hapo utamsikia Bwana akikuambia, “Leo, imenipasa niwe nyumbani mwako.”
BARIKIWA

Categories:

Leave a Reply