WANACHAMA wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) nchini kupitia vyama vya Akiba na Mikopo (Saccos) wataanza kupata mikopo ya nyumba na masuala mengine ya maendeleo kuanzia Julai mwaka huu, ilifahamika jana. Ofisa Mipango Mkuu wa NSSF , Gerald Sondo alisema hayo jana alipoeleza mikakati mbalimbali ya mfuko huo katika kuboresha maisha ya wanachama. Sondo alisema NSSF imejipanga kuwakopesha wanachama fedha nyingi kwa ajili ya ujenzi wa nyumba zao, elimu na hata biashara na kwamba mkopo huo utapitia Saccos za wanachama mahali pa kazi. “Kima cha chini kuikopesha Saccos kitakuwa Sh 50 milioni, lakini cha juu kinafikia hadi Sh 1 bilioni’’ alisema opfisa huyo akiwa kwenye Viwanja vya Maonyesho vya Mwalimu Nyerere maarufu kwa jina la Sabasaba mtaa wa Barabara ya Kilwa. Alisema maandalizi ya kuanza kutoa mikopo imekamilika na kwamba NSSF inatarajia kuanza kutoa fedha kuanzia Julai Mosi na kwamba taarifa kuhusu mpango huo zilishatyolewa kwa wadau wakati wa mkutano uliofanyika Arusha mapema mwaka huu. Kuhusu masuala ya riba, Sondo alisema NSSF itahakikisha inatoa riba ndogo kwa Saccos na kwamba ni martarajio yake kwamba wanachama nao watapata fedha hizo bila ya kuwa na riba kubwa kama za vyombo vingine vya fedha. Alitoa wito kwa wanachama NSSF kuunza Saccos mahali pa kazi na kujiwekea akiba nyingi ili waweze kukopa fedha hizo ambazo malengo ni kuwasaidia wanachama ili kuboresha maisha yao. Chanzo: Mwananchi

Categories:

Leave a Reply