Leo tutaangalia njia mbalimbali za kukusaidia unapopatwa na matatizo.
Mara nyingi mtu anapopatwa na matatizo hubabaika na kujikuta hana msaada wowote.
Mtu huyo huwa anashindwa kujikubali kama yupo salama na lipo tumaini jipya baada ya matatizo hayo anayokabiliana nayo.
Ni watu wachache wanaojikubali kuwa wana matatizo na kutafuta njia ya kukabiliana nayo.
Wengi walio na misukosuko hukosa furaha na kujiona kuwa ni wanyonge, waliokataliwa na jamii inayowazunguka.
Hali hiyo huwafanya afya zao kuzorota na kukabiliwa na magonjwa mbalimbali kama ya moyo na vidonda vya tumbo.
Kutokana na hali hiyo inayomkabili mtu huyo, jamii, ndugu na hata marafiki zake huwa mbali naye na kuacha kutoa ushirikiano wa karibu kwake.
Ni vizuri kuelewa kuwa, kila mmoja wetu ana matatizo, hivyo njia ya kuyatatua anayo yeye mwenyewe.
Unaporuhusu hali ya kukata tamaa kujengeka katika maisha yako, ndipo unapoona kuwa matatizo hayatatuliki na ni mzigo mkubwa usiobebeka.
Pili inakupasa kujua kuwa, matatizo ni kitu kisichoepukika katika maisha, japo yanaumiza sana kwa wakati huo.
Lakini faida yake ni kwamba yanakujenga sana imani yako na hata kuwajua watu wa kweli kwako, iwe ndugu ama marafiki.
Na huu ndiyo wakati muafaka wa kujenga maisha yako na kuimarisha ujasiri. Hakuna mtu mwenye akili na jasiri kama mtu mwenye matatizo, kwani fikra zake siku zote ni kutatua hali hiyo inayomkabili. Wakati wale wasio na matatizo hujibweteka kiakili hata kiafya.
Tatu, ni vema kuelewa kuwa njia ya kutatua matatizo yako unayo mwenyewe na lipo tumaini.
Hetu tuangalie mfano wa mtu anayekabiliwa na matatizo ya kuuguliwa na mtoto, baba mzazi na wakati huo huo anakuwa na madeni yaliyomwelemea na kumfanya ashindwe kuelewa anaanzia wapi.
Kumbuka kipindi kama hiki wapo baadhi ya ndugu na marafiki wanaokucheka, wakisubiri waone mwisho wa kushindwa kwako.
Njia sahihi za kufuata ni kuepuka sana kuwa karibu na watu kama hao. Kama unadaiwa na unakwenda kumueleza mtu asiye na madeni akusaidie shida yako, hatakuwa na moyo, atakucheka na wengine hufika mbali kwa kukutangaza.
Ni vizuri ukawa na watu walio na utayari wa kukusaidia, pata muda mzuri wa kupumzika ukiwa peke yako ili uwe na akili tulivu, utafakari uanze na tatizo lipi ili kukabiliana na hali uliyo nayo.
Si vizuri kumwambia kila mtu matatizo yako, kwani walio wengi hawawezi kukuzungumzia mambo mema kwa kuwa midomo yao imejaa hila.
Uwaone viongozi wako wa dini kwa ajili ya ushauri zaidi.
Pia kila unapokutana na watu wa aina mbalimbali jifunze kuongea nao vizuri na penda kuongelea zaidi mafanikio yako kuliko matatizo.
Hii inasaidia wale wasiopenda mafanikio yako, wasijue undani wako ulivyo.
Siku zote za maisha yako uwe na ndoto za mafanikio, hii itakufanya siku moja uketi pamoja na wakuu wa nchi. Kubali kupokea baraka kutoka kwa wengine na uwe mtu wa shukrani. Hiyo ni siri tosha ya kuondoa matatizo.
Tumia muda wako vizuri kupanga mambo ya kimaendeleo. Pia fanya mazoezi ya viungo na si kunywa pombe ukidhani kuwa utatuliza mawazo.
Kumbuka watu waliokabiliana na matatizo makubwa ndio walioweza kufikia mafanikio makubwa kiroho, kiuchumi na kisiasa, kwa kuwa wanazikubali changamoto katika maisha.

Categories:

Leave a Reply