NI vizuri ukakabiliana na hali ya wasiwasi inayokusumbua na kuanza siku mpya. Wasiwasi mara nyingi unasababisha uso wako kuharibika, kukunjika, kupatwa na chunusi, vipele vidogo vidogo, ngozi kukunjamana, nywele kubadilika rangi na wakati mwingine kukatika.
Unaweza kuona hali hiyo kuwa ni ya kawaida, lakini sivyo unavyofikiri, hivyo unaweza kukabiliana nayo kwa kuondoa hali hiyo ya hofu na wasiwasi.
Je, unapenda maisha? Je, unapenda kuishi maisha marefu na kufurahia afya bora? Unatakiwa kuwa na amani ndani ya moyo wako ambayo itakuwezesha kuishi kwa kujiamini.
Tuangalie mfano wa kijana Dave, ambaye alihakikishiwa na daktari wake kuwa ana ugonjwa wa kansa, hivyo tangu wakati huo alijiona kama anakufa taratibu kutokana na ugonjwa huo uliompata.
Kwa kuwa alikuwa bado kijana, hakupenda kufa mapema, hivyo kila mara akawa anasumbuliwa na hofu ya kifo. Hivyo aliamua kumpigia simu daktari wake na kumweleza hali aliyonayo na jinsi anavyojisikia kutokana na hali hiyo.
Daktari yule alimweleza wazi kijana Dave, kwamba, kama ataendelea kuwa na hofu, atakufa, cha msingi akubaliane na hali ile aliyokuwa nayo ya ugonjwa bila kuwa na wasiwasi.
“Ni kweli umepatwa na hali mbaya, cha msingi ikubali hali hiyo,” alisema daktari yule na kumsisitiza zaidi kwa kumwambia aiondoe hali ya hofu aliyonayo.
Tangu hapo Dave aliikubali hali ile na kuiambia nafsi yake hana haja ya kuwa na wasiwasi tena, wala kulia, pia yuko tayari kukabiliana na hali yoyote katika maisha.
“Sitaki kuwa na mawazo kuwa nina kansa, bali ninaamini kuwa akili yenye uchangamfu inausaidia mwili kupigana na magonjwa,” alisema Dave na hapo aliendelea kuwa na afya njema, na kusema kuwa anaufurahia msemo unaosema, ‘kubaliana na ukweli, ondoa wasiwasi, halafu fanyia kazi hali hiyo’.
Ni jinsi gani ya kuchanganua na kutatua matatizo yanayosababisha wasiwasi? Kwanza yakupasa upate uhakika wa jambo linalokusumbua, ulichanganue na kufikia uamuzi ambao utaufanyia kazi.
Unafikiri ni kwanini ni muhimu kupata uhakika? Ni kwa sababu kama una uhakika wa lile unalotaka kulitatua haitakuwa rahisi kupata utatuzi wa busara, kwani bila uhakika yote utakayoyafanya yatakuchanganya zaidi.
Unapoamua kutafuta utatuzi wa tatizo lako kamwe usigeuke nyuma na kuangalia hali uliyokuwa nayo awali, ambayo inaweza kukusababishia hofu nyingine. Pia tuangalie ni jinsi gani unaweza kuondoa hofu inayokukabili katika biashara zako.
Dk. Jarome anasema kuwa, kwa miaka 15 amekuwa akitumia nusu ya muda wake wa kufanya biashara zake kwenye mikutano, kujadili matatizo. Kwamba biashara hiyo inaweza kufanywa hivi au vile au kutokufikia muafaka. Anaeleza mara zote amekuwa akipata wasiwasi yeye na wenzake, kwenye viti walivyokalia vinavyozunguka, kutembea kwenye korido, kujadili na kuangalia ukubwa wa tatizo. Na inapofika usiku tayari amekuwa amechoka.
Anasema anategemea hali hiyo ya kuwa na mambo mengi yanayomkabili itakuwa inaendelea katika maisha yake yote. Anasisitiza amekuwa akifanya hivyo miaka 15 iliyopita, kamwe haitatokea kwake njia nyingine ya kufanya hivyo.
“Hapa kuna siri,” anasema Jarome. “Kwanza nimeacha utaratibu niliokuwa nimejiwekea katika mikutano kwa miaka 15 iliyopita.” Anasema aliamua kubadilisha mfumo huo na kuwashirikisha wengine kwa kuwauliza watafanya nini ili kutatua matatizo.
Pili, anasema alitengeneza sheria mpya ya kwamba kila mmoja atakayetaka kupeleka tatizo kwake, lazima ajiandae na kuandaa taarifa ambayo itampatia majibu katika maswali manne ambayo ni kutaka kujua tatizo haswa ni nini, chanzo chake, njia zinazowezekana kutatua tatizo hilo na njia za kutatua tatizo zitakazofikiwa. Hiyo ndiyo changamoto ya kuondoa wasiwasi kwa asilimia 50.
Ni jinsi gani ya kuondoa hali ya wasiwasi inayokukabili kabla haijakuondoa wewe? Tuangalie mfano wa Steven ambaye alikuwa jasiri na kuwaeleza wenzake aliokuwa akisoma nao kwenye chuo kimoja, jinsi ambavyo alikumbana na msiba mara mbili katika familia yake. Kwa maelezo ya Steven, mara ya kwanza alimpoteza mtoto wake wa miaka mitano ambaye alikuwa ni binti, mtoto aliyempenda mno.
Anasema yeye na mke wake walifikiri kuwa hawataweza kustahimili hali hiyo, lakini Steven anasema, miezi kumi baadaye, Mungu aliwapa mtoto mwingine wa kike ambaye alifariki baada ya siku tano.
Steven alisema yeye na mkewe hawakuwahi kupitia kipindi kigumu kama hicho katika maisha yao. “Sikuweza kuchukuliana na hali hiyo, sikuweza kulala, sikuweza kula, sikuweza kupumzika wala kuburudika. Mishipa yangu ilikuwa ikitetemeka na hali ya kujiamini ikaniaondoka,” anasema baba huyo.
Mwishoni alienda kwa madaktari ambao walimshauri wamchome sindano ya usingizi au atafute matembezi ya mbali kwa ajili ya kupumzisha akili. Anasema alijaribu vyote lakini havikuweza kumsaidia.
Anasema hali hiyo iliendelea kumtesa kwa muda mrefu, akaeleza kuwa kwa yeyote aliyewahi kupooza kutokana na jambo baya lililompata ataelewa ni nini anachokisema.
Lakini anamshukuru Mungu kwa kuwa, alikuwa na mtoto mmoja aliyebakia wa kiume wa miaka mitano. Ambaye alimpa ufumbuzi wa tatizo lake. Siku moja mchana alipokuwa amekaa anajisikitikia, mtoto huyo alimwuliza baba yake kama anaweza kumtengenezea boti.
“Ukweli ni kwamba nilikuwa sijisikii kutengeneza boti hiyo, nilikuwa sijisikii kufanya jambo lolote lile,” alisema na kuongeza kuwa ilimbidi afanye hivyo kwa kuwa mtoto wake huyo huwa abadili msimamo wa kile anachokitaka, hivyo ilimbidi amtengenezee.
Anasema kutengeneza boti hiyo ya kuchezea ilimchukua muda wa saa tatu. Lakini ilipokwisha, aligundua muda huo alioutumia uliweza kumpumzisha akili yake na kumpa amani aliyokuwa nayo kwa muda mrefu.
Hivyo amegundua kuwa unapokuwa na shughuli za kufanya kipindi ambacho umekuwa katika wakati mgumu uliokufanya uwe na wasiwasi, hofu au hali ya kukata tamaa, zinakufanya mtu uwe na nguvu mpya kwa kuwa hupati muda wa kufikiri yaliyopita, bali jinsi ya kufanya kazi hiyo ili ikamilike. Hivyo alifikia uamuzi wa kujishughulisha ili hali aliyokuwa nayo isimrudie tena.
Makala hii imetafsiriwa kutoka kwenye kitabu kijulikanacho kama ‘Ondoa wasiwasi anza maisha mapya’, pamoja msaada wa intaneti.
source dada lucy Ngowi,

Categories:

Leave a Reply